NLD YATUPIA KARATA YAKE ISMANI NA KATA TANO, YATARAJIA USHINDI MKUBWA
Na Mwandishi Wetu
Chama cha siasa cha National League for Democracy (NLD) kimetangaza kuingia kwa nguvu katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Ismani mkoani Iringa pamoja na uchaguzi wa madiwani katika kata tano tofauti nchini.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa NLD, Doyo Hassan Doyo alisema chama hicho kimekamilisha maandalizi ya kampeni kuelekea uchaguzi unaotarajiwa kufanyika Juni 1 mwaka huu.
Katika uchaguzi wa ubunge wa Jimbo la Ismani, NLD imemsimamisha Subira Majuto Kalolo ambaye atashindana na wagombea wengine 16 waliopitishwa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC).
Doyo alisema chama hicho kina imani na mgombea wake kutokana na uwezo wake wa kuzungumzia masuala ya maendeleo na kusikiliza changamoto za wananchi wa Ismani. Alieleza kuwa kampeni za NLD zitajikita katika sera za maendeleo, ushirikishwaji wa wananchi na utatuzi wa changamoto za kijamii na kiuchumi.
Kwa upande wa uchaguzi wa madiwani, NLD imetangaza wagombea wake katika kata tano.
Rajab Kisuko-Kata ya Mzimuni
Meshack Masuguliko-Kata ya Zongomera
Laylat Godliver-Kata ya Itilo
Asha Milongea-Kata ya Kibiti
Ramlat Abdul-Kata ya Bongera
NLD imesema itaendesha kampeni za karibu na wananchi kwa lengo la kusikiliza matatizo yao na kutoa suluhisho la changamoto zinazowakabili. Chama hicho pia kimewahamasisha wananchi kushiriki kwa wingi katika mikutano ya kampeni na kujitokeza kupiga kura siku ya uchaguzi.
