Breaking News

Mpina Apokewa Kwa Shangwe Mkutano Mkuu wa ACT Wazalendo



Kada mpya wa ACT Wazalendo na mbunge wa zamani wa Kisesa, Luhaga Mpina, amezua shamrashamra katika Mkutano Mkuu Maalumu wa chama hicho unaoendelea Mlimani City, Dar es Salaam.


Na mwandishi wetu Kelvin Kijo

Mpina aliingia ukumbini kwa mshangao wa wajumbe waliokuwa wakimfuatilia kupitia runinga, wakati Onesmo Ole Ngurumwa wa THRDC alikuwa akizungumza. Kuingia kwake kulivuruga utulivu, huku wanahabari wakimiminika eneo lake kwa picha.


Kutokana na hali hiyo, Katibu Mkuu Ado Shaibu alilazimika kubadili ratiba na kuharakisha utambulisho wa watiania wa urais, hatua iliyotokana pia na hoja ya Msajili Msaidizi wa Vyama, Sisty Nyahoza. Watiania waliotambulishwa ni Othman Masoud, Aaron Kalikawe na Mpina, ambaye alipokelewa kwa shangwe kubwa zaidi.


Baada ya utambulisho, Zitto Kabwe alialikwa kutoa hotuba, na mkutano ukaendelea kwa utulivu. Kura za maoni zinatarajiwa kupigwa baadaye leo ili kumpata mgombea rasmi wa urais kwa uchaguzi wa Oktoba 2025.

Mkutano huo umeendelea kwa msisimko mkubwa kutokana na ushindani wa watiania na uhamasishaji wa wanachama.