Breaking News

WAWEKEZAJI WAITWA KUWEKEZA SINGIDA NA DODOMA




Na. Wellu Mtaki, Dodoma 


Mikoa ya Singida na Dodoma  ina fursa nyingi kwenye  kilimo ,viwanda pamoja na ufugaji ikiwemo Ufugaji wa Nyuki  hivyo wawekezaji  wameaswa kuwekeza Katika mikoa hiyo Ili kujiongezea kipato na kukuza uchumi wa Nchi.


Hayo ameyasema Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya uwekezaji na maeneo maalum ya kiuchumi (TIZESA)  Gilead Teri wakati anazungumza na waandishi wa habari katika mwendelezo wa maonesho ya wakulima, Nanenane yanayofanyika Zunguni Jijini Dodoma huku akibainisha kuwa ushiriki wao wa kongamano la uwekezaji la Kanda ya kati umelenga kuhabarisha Umma kuhusu fursa zinazopatina Katika Mikoa hiyo.


Pia Mkurugenzi huyo ameongeza kuwa  kongamano hilo lililenga  kufanya utambulisho wa TIZESA upya kwa wawekezaji wa Kanda ya kati na kutoa habari njema ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan ambaye amewapa jukumu la kuwa kituo cha pamoja cha uwekezaji.




Aidha amesema Kuwa tarehe 12 Agosti Mwaka huu watazindua huduma mpya za uhamasishaji na uwekezaji ndani ya TIZESA  ambapo wataanza na maeneo (5) ambayo ni pamoja na Benjamin mkapa Dar- Es- Salaam, Bagamoyo hekari 150, Kwala hekari 100 Dodoma hekari 600 pamoja na Buzwagi ambapo wanatarajia utazinduliwa na  waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Mipango na uwekezaji Profesa Kitila Mkumbo.

 

Naye mwakilishi msaidizi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa  Mataifa (FAO)  Charles Tulahi amesema kuwa  Wanaratibu miradi mbalimbali nchini Tanzania ambapo kwa Dodoma  wanawezesha wanawake kiuchumi.


Kati ya mradi wanaoutarajia  kuanzishwa ni pamoja na kilimo cha tende Mkoani Dodoma hivyo wakulima wa sekta mbalimbali watawekeza na kuleta mageuzi kwasababu tende zilikuwa zinaagizwa kutoka nje.


Hata hivyo Tulahi amewaasa watanzania kuwekeza katika kilimo katika sehemu mbalimbali zenye mnyororo wa thamani kwasababu Duniani kote idadi ya watu imekua na uhitaji wa Mazao ya kilimo pia yamekua hivyo uwekezaji kwenye kilimo unatija kubwa.