ZUNGU AITAKA KARIAKOO FESTIVAL KUZUNGUKA WILAYA ZOTE
Na Mwandishi wetu DSM
Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mbunge wa jimbo la Ilala, Mussa Azzan Zungu amewataka wafanyabiashara wa Kariakoo kuendeleza maonesho ya wafanyabiashara wa wilaya zote nchini Tanzania.
Agizo hilo amelitoa wakati alipotembelea maonesho ya wafanyabiashara wa kariakoo yaliyopewa jina la Kariakoo Festival yanaondelea katika viwanja vya Mnazimmoja jijini Dar es salaam.
“Niwapongeze wafanyabiashara kwa kuamua kukaa pamoja lakini pia kuweza kufanya biashara pamoja hususani biashara za mtandaoni kwasababu ndicho kilio kikubwa cha Rais cha kutaka kuona wafanyabiashara wanakaa pamoja na kulipa kodi kwa wakati” amesema Zungu.
Amesema ni vyema kwa maonesho haya kuzunguka wilaya zote ili kutoa fursa kwa wafanyabiashara kuweza kuonesha biashara zao lakini pia kutoa elimu kwa wateja, kupata elimu kwa taasisi za serikali ikiwemo TRA, FCC, UTT AIMS, BRELLA,TBS pamoja na NHIF.
“Kipekee niwapongeze NMB kwa kua ndio wazamini wakubwa wa kariakoo Festival na kuwataka mashirika mengine kuiga mfano wa NMB kwa kuwasapoti wafanyabiashara Katika maonesho mbalimbali”amesema Zungu.
Hata hivyo amewashauri wafanyabiashara kujiunga na mfuko wa bima mapema wasisubiri kuumwa kwani kujiunga mapema ni kusaidiana hasa kwa wale wa hali ya chini.
Aidha amemshukuru Rais Samia kwa namna ya kipekee kwa kuwaunganisha wafanyabiashara nguvu ya kufanya kazi kwa pamoja kwa sababu kulikuwa na shida kubwa sana ya wafanyabiashara wa kariakoo maduka makubwa na wamachinga lakini akafanya kila jitihada ya kuwaunganisha pamoja.
Hata hivyo amewapongeza wafanyabiashara kwa kuwa na maono makubwa yakulipa kodi kwakua kodi ndio zinazoleta maendeleo ya nchi ikiwemo kujenga barabara ya mwendokasi, Treni ya Umeme, Daraja la Magufuli na miundo mbinu mingine







